LATEST POSTS

Friday, December 9, 2016

MBILIA BELL ET L'AFRISA INTERNATIONAL-TAFSIRI YA WIMBO NAKEI NAIROBI BY OCHOLA ARUM



                                        MBILIA BELL.


                     Wimbo:-Nakei Nairobi (Naenda Nairobi)
                     Msanii:-Mbilia Bell
                     Mahali:-Congo DRC

--Nayoki Nzambe motindo ya mpasi banyokoliyo
Oh! Mungu nimesikia uchungu mwingi walivyo kutesa

--Yaka pembeni nazalise wayo ya motema
 Sogea karibu bado uko moyoni

--Tovandi bomwana tomesani ngai nayo  Donoui.
 Toka tukiwa watoto tuliishi Pamoja

Tobandi bomwonaki  moninga na miso ya mama
 Tulianza kuonekana marafiki machoni mwa mama zetu

--Ezali mabe nayoka okomi na mpasi naza te
Nimesikia habari mbaya kuwa umepata mateso mengi wakati sipo

--Nakoya na Kenya naya kozwa yo tozonga na Kinshasa
Nakuja Kenya naja nikuchukue turudi Kinshasa

--Ya elodie mapasa lokumu ya famii boti wapi!?
Tulikuwa kama napacha heshima ya familia uko wapi?

                                            MUZIKI

--Kicamarade ya bomwana tango mosusu elakaka bondeko
Urafiki unaoanzia utotoni wakati mwingine ni nzuri kuliko undugu

--Toyebani Bomwana totamboli Kenya mobimba ngai na yo
Tulifahamiana toka utotoni na kutembea Kenya yote Mimi na wewe

Nairobi Mombasa Nakuru kisumu toyebani
Nairobi Mombasa Nakuru kisumu tulifahamika

                                              MUZIKI

              Chorus
                              Nakei Nairobi mpo nasalisa Dunoui
                              Naenda Nairobi ili nimsaidie Duni

                               Nakei Nairobi nakozonga na Dunoui
                               Naenda Nairobi ili nirudi na Duni.

                                         -----MWISHO----

NB-WIMBO NAKEI NAIROBI NA WIMBO TWENDE NAIROBI NI NYIMBO MBILI ZENYE MAUDHUI TOFAUTI BALI MIDUNDO SAWA SAWA,MTUNZI ALITUMIA MIDUNDO YA NAKEI NAIROBI KWENYE WIMBO TWENDE NAIROBI AMBAPO ALIALIKWA KWENYE SHEREHE YA MIAKA 21 YA UHURU WA NCHI YA KENYA.

Saturday, September 3, 2016

MUZIKI WA DANSI NI AJIRA YA WENGI,UKIYUMBA NA WENGI WANAYUMBA,ASEMA FAIDA ONGALA.



          MGENI WETU HII LEO NI FAIDA ONGALA WA AKUDO IMPACT


                                                Faida Remmy Ongala.

Blog pendwa ya Kavasha leo imepata bahati ya kukutana na mwanamuziki anaekuja kwa kasi ambae pia ni binti wa  mwanamuziki mkongwe wa miondoko ya dansi Marehemu Dokta Remmy Ongala,huyu si mwingine bali ni Faida Ongala,Kavasha Blog ilikua na machache iliyohitaji kujua toka kwake kwa ajili ya wasomaji wa wake na mazungumzo yalikua kama ifuatavyo;


1.Kavasha Blog;  Dada Faida wasomaji wa blog hii pote duniani wangependa kujua mawili matatu toka kwako,wewe ni nani na historia yako ya muziki mpaka sasa,bila shaka upo tayari kutujuza,karibu sana.

Faida;  Asante sana nipo tayari kuwajuza,Mimi naitwa Faida Remmy Ongala,ni miongoni mwa watoto wa Marehemu mwanamuziki Dokta Remmy Ongala,nilipenda muziki toka zamani nikiwa mdogo,nilivyomaliza masomo ya Sekondari nilijiunga na chuo cha muziki kiitwacho Evelyne Music School kilichopo Kimara bucha baada ya kusoma miezi mitatu nikahamia chuo cha DHW Country Music  Academy kilichopo Zanzibar baada ya kuona kuna unafuu wa ada,Nashukuru Mungu baada ya kuwa nafanya vema katika masomo nikapata wafadhili ambao walinisomesha bure kipindi chote ambachonilikua nikisoma hapo,nilisomea kupiga gitaa na ngoma za asili na kucheza pia na baada ya Chuo hicho cha Zanzibar nilikwenda Ethiopia ambapo nilisoma kwa miezi minane ambapo mpaka sasa nimemaliza masomo kwa jumla ya miaka mitatu ya masomo mbalimbali ya muziki kama nilivyoyataja katika vyuo vyote vitatu toka Dar,Zanzibar hadi Ethiopia.
                  Faida Ongala akifanya mazoezi nyumbani kwake.

2.Kavasha Blog;  oohh historia nzuri kabisa bila shaka ni mwanamuziki msomi Faida

Faida;anacheka….asante ni msomi kiasi ,yafaa sisi wanamuziki tupate elimu kidogo juu ya muziki ili kujua kwa undani muziki ukijumlisha na vipaji vyetu.

3.Kavasha Blog;  Ni nini ulichokipata kutoka kwa baba yako marehemu Dk Remmy Ongala kuhusiana na muziki?

Faida anajibu;Nimejifunza na kupata vitu vingi toka kwa baba angu mzee Remmy kama vile kufanya juhudi katika kazi yangu ya muziki  kitu ambacho nakifanya ili kuweza kufikia mafanikio yake yeye ama mara mbili zaidi ya pale alipofikia,kitu kingine alipenda kazi yake na mie pia ninaipenda kazi yangu katika mazingira na namna zote zile na kingine nimerithi kipaji chake cha muziki na kuwa mwanawe wa kike wa pekee niliye katika fani hii ya muziki. 


                           Baba wa Faida,Dr Remmy Ongala.

 4. Kavasha Blog;  Ni muziki gani unaumudu ?

Faida;Namudu miziki mingi na sipigagi miziki michache kama singeli,hiphop,taarab,michiriku nk.

5. Kavasha Blog;  Baba yako Dk Remmy alitumia kauli kali kutetea alichokiamini  mfano wimbo muziki asili yake wapi kuna maneno haya’’muziki sio uhuni,kama muziki ni uhuni kwa nini unanunua kaseti,unacheza muziki ama unaomba nyimbo redioni,je unawaambia nini wanaodhani muziki ni uhuni?

Faida; Ni kweli muziki sio uhuni,muziki ni kazi kama kazi nyingine na inapaswa kuheshimiwa na watu wasifikiri kuwa kila afanyae muziki ni muhuni la hasha,uhuni ni asili ya mtu ndio maana watu wanaofanya kazi katika ofisi zenye heshima utakuta ni wahuni,vizazi vya washika dini navyo utakuta kuna wahuni waliobobea na hata watoto wa matajiri wasio na shida ya chochote utakuta ni wahuni kupita wanamuziki hivyo napenda wadau wa muziki na wale walio nje ya muziki wafahamu kuwa muziki sio uhuni ni kazi nzuri na ya ujuzi mkubwa kama ama zaidi ya kazi ya baadhi ya wanobeza kazi ya muziki.

        Faida Ongala akijiandaa kupanda jukwaani Nchini Dubai.

6. Kavasha Blog;  Vipi kuhusu familia umeolewa?

Faida;Mimi sijaolewa na sina mtoto,ninaishi na familia yangu inayojumuisha mama na ndugu zangu wengine.
7. Kavasha Blog;  Uliwahi kufanya kazi na bendi ama makundi gani na sasa upo na  kundi gani?

Faida; Niliwahi kufanya kazi na kundi la kaka zangu Godfrey na Thomas katika Band yao inayojulikana kama Ongalas Band ,nikatoka kwa kaka zangu ili kujitafutia changu mwenyewe maana kutegemea cha ndugu sana ni tatizo na pia kuongeza uzoefu ambapo nilikwenda Dubai kujiunga na Band iitwayo 2extra Ngwasuma ambapo nimerudi na kujiunga na Band ya Akudo Impact vijana wa masauti,pia ninaweza kupiga kama solo artist,nimepita pia kundi la ndege watatu kwa muda mfupi.

               Hili ni kasha la wimbo wake wa UMEBADILIKA.

 8. Kavasha Blog;  Unaonaje maendeleo ya muziki hususani wa dansi nchini?

Faida; Kusema kweli muziki kwa hapa Tanzania umeshuka kiwango hasa muziki wa dansi,unajua muziki wa  dansi unategemewa na wanamuziki wengi na hata wasio wanamuziki kwa sababu unatoa ajira kwa watu wengi kwa wakati mmoja kuliko aina nyinginezo za muziki kama vile Bongofleva nk, hivyo muziki wa dansi unavyoendlea kushuka inakua mbaya sana kwa wanamuziki na wadau kwea namna moja ama nyingine.

9. Kavasha Blog;  Tangu kifo cha Mzee wako Dokta Remmy ile staili yake ya kutoa usia na kukemea maovu katika jamii na kupongeza wale waliofanya mazuri na wenye uthubutu hakika imepotea,ukiwa wa damu yake una mpango wa kufata nyayo zake?

Faida;Ndio nina mpango huo kwa sababu nilikua napenda alivyokua anawaambia ukweli watu na viongozi wazembe,mfano wimbo niseme nini ambao anasema ‘’saa mbili asubuhi,foleni kwenye supu,ofisi ipo na nani bwana weee’’ukiangalia wanamuzki wengi hasa wa kizazi kipya(bongofleva)wamejikita zaidi kwenye nyimbo za mapenzi lakini mimi nitafata nyayo za baba ili niweze kuelimisha wananchi katika jamii na walimwengu kwa ujumla kama alivyofanya baba.
          Marehemu Dokta Remmy Ongala wakati wa uhai wake.

10. Kavasha Blog;  Nini malengo yako ya baadae?

Faida anajibu; Natarajia kuwa mwanamuziki mkubwa sana kitaifa na kimataifa,pia niweze kufikia malengo yangu ninayoyawazia na kufanya vizuri katika tasnia hii ya muziki.
               Faida Ongala akipozi wakati wa mapumziko.

11. Kavasha Blog;  Unawaambia nini wadau,Serikali na wanamuziki kwa ujumla kuhusu kuinua muziki wa dansi na mingine kwa ujumla?

Faida anajibu;Jamani muziki wa dansi ni muziki wa toka enzi na enzi,umetumika sana katika shughuli za kitaifa na kimataifa kama wimbo Zimbabwe wa DDC Mlimani Park ukizungumzia uhuru wa Zimbabwe,naiomba serikali wajaribu kukaa na wadau wa muziki na wanamuziki kuangalia nini cha kufanya ili kurudisha hadhi ya muziki wa dansi nchini,pia nawaasa wanamuzki wote kuwa kitu kimoja bila kujali tofauti za makundi yao,ushrikiano ni jambo la msingi katika maendeleo yetu na pia kuupandisha muziki huu wa dansi.

Kavasha Blog;  Tunakushukuru Lady Doctor Faida Ongala kwa ushirikiano wako natumai tutaendelea kuwa pamoja siku zote.

Faida ;Asante na mie nafurahi kuzungumza na Blog ya kundi la Kavasha Group Tanzania.

                        KILA LA HERI DADA FAIDA ONGALA      
                ANAPATIKANA KWA SIMU NAMBA  ZIFUATAZO
                            +255715023646 KIKAZI ZAIDI.

Monday, August 8, 2016

MIAKA 12 BAADA YA KIFO CHA BALISIDYA,MFAHAMU KWA UFUPI.

KUMBU KUMBU YA MIAKA 12 TANGU KUFARIKI KWA MWANAMUZIKI MKONGWE NA MAHIRI NCHINI,MAREHEMU PATRICK MARTIN YOHANA BALISIDYA NA HISTORIA YA BENDI YA AFRO 70-IMEANDALIWA NA DAUDI KISUGURU.
 
                                                              Marehemu Balisidya.

Ni miaka kumi na mbili imepita tangu kufariki kwa mwanamuziki huyu mkongwe na mahiri katika tasnia hii ya muziki wa dansi aliyewahi kuvuma ndani na nje ya mipaka ya TANZANIA.

Ni mwanamuziki aliyekuwa anavimudu vyombo vingi vya muziki kama kinanda,gitaa zote,utunzi,uimbaji na upangaji wa muziki,PATRICK BALISIDYA ni mwenyeji wa mkoa wa Dodoma alizaliwa Mwezi April,1946 na kupata elimu yake ya msingi katika shule ya MVUMI BOYS PRIMARY SCHOOL waka 1954 na kushindwa kuendelea na masomo baada ya kuugua na kushindwa kufanya mtihani wa mwisho wa darasa la nne na baada ya matibabu ilibidi arudie ili aweze kufanya mtihani wa mwisho wa darasa la nne kwa bahati nzuri akafaulu na kuendelea na masomo ya darasa la tano mpaka la nane katika shule ya CHILONWA MIDDLE SCHOOL na baada ya mtihani wa darasa la nane akachaguliwa kuendelea na kidato cha kwanza katika shule ya DODOMA SECONDARY SCHOOL baada ya matokeo ya kidato cha nne PATRICK BALISIDYA alichaguliwa kujiunga na DAR ES SALAAM TECHNICAL COLLEGE ( Dar Tech) kwa sasa kinafahamika kama DAR ES SALAAM INTERNATIONAL TECHNOLOGY kwa ajili ya kuchukua Diploma ya majumba na umeme.

Harakati zake na hamasa ya kuupenda muziki inaanzia nyumbani kwao,Baba yake mzazi MZEE MARTIN YOHANA BALISIDYA alikuwa na gitaa la box galatoni ambalo alikuwa analipiga kwa kujifurahisha hapo nyumbani na mama yake mzazi alikuwa anapiga kinanda kanisani nae pole pole akaanza kujifunza na alijifunza zaidi pale alipojiunga na Dodoma secondary,Shule ilikuwa na bendi yake iliyofahamika kwa jina la CHITOMDULI ambayo PATRICK ndiye alikuwa anaiongoza.

Kwa haraka aliyokuwa nayo hapo aliona anachelewa kuyafikia malengo yake aliyokuwa nayo akawa anatoroka kwenda kushiriki na bendi ya CENTRAL JAZZ BAND iliyokuwa na maskani yake  hapo hapo mkoani Dodoma ambayo ilikuwa inamilikiwa na mbunge wa serikali yaTanganyika wakati huo aliyefahamika kwa jina la STANLEY MSUVE, hiyo ilikuwa ni Mwaka 1964 hali hii ikampelekea kuingia kwenye mgogoro kati yake na walimu wake mpaka kufikia kufukuzwa Shule,habari zilipowafikia wazazi ikabidi waingilie kati na hatimaye suluhu ikapatikana na Patrick kuweza kuhitimu kidato cha nne mwaka 1965.


Ujio wake katika Jiji la Dar es salaam kuja kujiunga na chuo cha DAR TECH ndiyo ikawa fursa kwake ya yeye kupata nafasi ya kujiunga na Bendi ya Dar es salaam jazz kikosi "B" na hatimaye kuwa kiongozi wa Bendi hiyo ya pili na ile ya kwanza yaani DAR JAZZ "A" ikiongozwa nae KING MICHAEL ENOCK.Bendi hii ikatoa upinzani wa hali juu kwa ile ya "A" na kupelekea uongozi wa juu wa Dar es salaam jazz band kuamua kumpandisha daraja Patrick kumtoa "B" na kumpeleka "A" hiyo ilipelekea kufanya kazi pamoja na KING ENOCK, King Enock akipiga solo namba moja na Patrick akipiga solo namba mbili.


Mwaka 1968 Dar es salaam jazz band ikaanza kufifia kutokana na uchakavu wa vyombo hali hiyo ikapelekea Patrick balisidya kuomba ridhaa kwa baba yake ili amsaidie kuanzisha bendi yake mwenyewe na baba yake akaafiki na kumnunulia Box gitaa nne na baadhi ya vyombo vingine walichukua vile vya iliyokuwa CENTRAL JAZZ BAND  ambayo kwa wakati huo ilikuwa imeshasambaratika na huo ndiyo ukawa mwanzo wa kuundwa kwa  AFRO 70 BAND "wana afrosa" Bendi ambayo ilipoanzishwa ilifahamika kama LES VOLCASE mwaka 1969 lakini haikupata usajili kwa sababu jina hilo lilionekana limekaa kizungu zaidi na haliendani na uasilia wetu. 


Ndipo mwaka mmoja baadae yaani mwaka 1970 kupitia watangazaji wa wakati huo hasa TIDO MUHANDO alikuwa akiwaita hao kuwa ni vijana wa AFRO mtindo wa nywele ulio kuwa maarufu kwa wakati huo na wao wakaongezea 70 wakaamua kujiita AFRO 70 wakitumia mtindo wa "afrosa" baada ya mazoezi makali bendi ikazinduliwa tarehe 25/12/1969 katika ukumbi wa STEREO NIGHT CLUB lakini Bendi ilianzia Tandika mtaa wa "sambwisi".


Ule umaarufu aliokuwa nao wakati akiwa na bendi ya Dar Jazz Band ulimsaidia kupata mapokeo mazuri kutoka kwa mashabiki katika siku hiyo ya uzinduzi, baada ya uzinduzi na kufanya maonyesho kadhaa ikabidi bendi isafiri kuelekea nchini KENYA kwa ajili ya kufanya recording ya nyimbo zao na kwenda kuingia mkataba na kampuni ya A.I.T. yaani ANDREW INTERNATIONAL TRADING na kufanikiwa kurekodi kwa lebo ya motomoto tarehe 23/05/1971 walirekodi nyimbo kama "vick" ," dirishani" ,"afrika" ,"bembea", "monika" ,"muongozo wa Tanu" n.k.

 
Patrick Balisidya -solo na kuimba ,second solo - Master Owen Franis Liganga , Rhythm - Jackson Makangila ,Besi - Charles George Matonya ,Ngoma - Saidi Nassoro ,Tumba -Hemedi Issa Kang'ombe wengine ni Zuberi Msekeni Didi , Teddy Chilufya,Salumu Munisi , Bille William Senzighwa na Adam Sykes na Steven Balisidya.

 
Tarehe 29/09/1971 walitoa vibao kama "mapenzi ya mama" ,"magreth" , "makayele", "kenya mpya" ," anjelina" na "pesa".Baadae wakahamia katika kampuni nyingine ya KELCHO  kwa OLUOCH KANINDO inayofahamika kama A.P.CHAMBRANE na tarehe 30/12/1971 walitoa vibao kama "libondela" ,"tembea tembea" ,"mpenzi Lidya" ,"Baba na Mama waheshimiwe" n.k.
Walitoa tena vibao vingine kama "gema" ," nataabika" ,"tausi" ,"mavula" ,"harusi" n.k. Hapa waliongezeka wanamuziki kama Shabani Mbotoni - sax, Paulo Ndasha - drum na Dickson Unga - mwimbaji na Tarehe 23/04/1972 walitoa nyimbo kama "nakupenda kama lulu" ,"ukombozi wa afrika" ,"dada yatubidi" ,"wapi heshima" na "kabla hujafa hujaumbika" na tarehe 15/07/ 1977 walitoa nyimbo kama "mashaka" ,"shangwe" ,"nini kisichokuwepo afrika" ,"week end" n.k.Pia waliongezeka wanamuziki kama, Sophia Nzuki ,Anna Mbula ,Rehema Kapteni , Habibu Jeff Mgalusi, John Festory, Christopher Phabbiano (Chriss Phabby ) na George Silvester.
 

Uwepo wa bendi hii katika tasnia ya muziki wa dansi katika miaka hiyo ya sabini unakumbukwa kwani iliwahi kunyakua ubingwa wa mashindano ya bendi za vijana yaliyowahi kufanyika jijini Dar es salaam mwaka 1971, 1972, 1973 na 1974, haya mashindano ndiyo yaliyowafanya kupata tiketi ya kuiwakilisha Nchi Nchini NIGERIA katika mashindano ambayo yalikuwa yafanyike mwaka 1975 lakini pakatokea mapinduzi ya kijeshi Nchini humo na mashindano kusogezwa mpaka mwaka 1977 yakihudhuriwa na bendi mbalimbali kama TP OK JAZZ, BEMBEA JAZZ BAND ya Guinea, AFRISA INTERNATIONAL, BELLAFONTE, ANEKOLAPO KUTI n.k. na AFRO 70 BAND ikiibuka na ushindi wa pili.

 
Tarehe 25/12/1975 wakati wanarejea kutoka ngerengere walikokwenda kufanya onyesho la kujitambulisha kwamba wao ndiyo wawakilishi  wa Nchi  Nchini Nigeria,walipata ajali pale Ubungo sehemu iitwayo ROMBO,gari waliokuwa wakisafiria ilipinduka na kupelekea vyombo vya bendi kuharibika vibaya na kuomba kujitoa katika mashindano hayo,lakini serikali kupitia kwa Waziri wa Wizara ya utamaduni wakati huo MIRISHO SARAKIKYA iliamua kuwapa vyombo ilivyokuwa imevinunua kwa ajili ya kuanzisha Bendi yake ili wawakilishe Nchi.


Baada ya kurejea nchini Nigeria kwenye mashindano yaliyofahamika kama maonyesho ya mtu mweusi Bendi ikapata mwaliko nchini MSUMBIJI  uliodhaminiwa na RADIO MOZAMBIQUE kwa wakati ule na kuweza kufanya maonyesho matatu kwa ajili ya wahanga wa vita vya kumng'oa MRENO na kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi 40,000/= pesa ya Msumbiji kwa wakati ule.


Waliporejea kutoka msumbiji wakatakiwa  AFRO 70 BAND wafanye onyesho la Chama na Serikali Patrick akadai malipo kwanza ndiyo afanye onyesho hali iliyopelekea kuingia kwenye mzozo mkubwa kati yake na serikali mpaka kupelekea kunyang'anywa vyombo, vyombo ambavyo ndivyo vilivyoanzishiwa bendi ya ASILIA JAZZ BAND naye Patrick Balisidya kufungua kesi ya madai mahakakani kesi ambayo inaendelea mpaka leo.
 

Lakini kwa bahati mbaya  Patrick alianza kusumbuliwa na maradhi yaliyopelekea kifo chake hapo Tarehe 08/08/2004 na kuzikwa tarehe 12/08/2004 katika makaburi ya Buguruni Malapa na kuiacha kesi yake ya madai mikononi mwa mdogo wake aitwaye FREEDOM BALISIDYA na huo ndiyo ukawa mwisho wa uwepo wa bendi ya AFRO 70 BAND na kutoweka katika ulimwengu huu wa tasnia ya muziki wa dansi.
 

Patrick Balisidya enzi za uhai wake baada ya AFRO 70 kutoweka aliwahi kufanyakazi na ORCHESTRA SAFARI SOUND "masantula"  na kupiga kinanda kwenye wimbo wa "niambie siri"  na THE RAIN BOW CONECTION Bendi iliyokuwa inapiga muziki wake pale NEW AFRICA HOTEL na Mwaka 1979 alienda Nchini SWEDEN na kufanikiwa kutoa albamu moja iliyoitwa "bado kidogo".
 
Patrick katika uhai wake aliwahi kufunga ndoa na BI SOPHIA NZUKI na walibahatika kupata mtoto mmoja wa kike aitwaye MAWANDO PATRICK BALISIDYA.

BWANA AMETOA NA BWANA AMETWAA.
 
JINA LA BWANA LIHIMIDIWE - AMIN.



                                                    R.I.P PATRICK BALISIDYA

Monday, July 25, 2016

MZEE ZAHIR ANENA JUU YA WIMBO TUMERUDI KISHUJAA

                                                     MASHUJAA DAY

Ikiwa leo ni siku ya kukumbuka mashujaa wetu waliopigana katika vita vya Kagera dhidi ya majeshi ya uvamizi ya nduli Idd Amin Dada,Ukurasa huu wa Kavasha ulipata nafasi ya kuongea kwa ufupi na afande mstaafu na mwanamuziki nguli wa zamani wa Bendi ya Kimulimuli Mzee wetu Zahir Ally Zorro ambapo tuliweza kumuuliza maswali machache kama ifuatavyo;
           Pichani:Mzee Zahir akipokea tuzo toka kwa Mhe;Jakaya Kikwete.

1.Nini ilikua dhima ya wimbo wako wa Tumerudi kishujaa?

Jibu-Ni wajibu mwema uliotekelezwa vyema,mashujaa walioanguka,mashujaa waliorudi,kwetu sisi askari ilikua kielelzo tosha kuhusu utekelezaji usio na shaka wa amri ya Amiri jeshi wetu mkuu wakati huo Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ambae mpaka kifo chake alisisitiza kuwa tutaenzi juhudi za mashujaa wetu milele.

2.Lini ilikua mwanzo kabisa kuimba wimbo huo hadharani?

Jibu-Ilikua mwezi wa August 1978 niliuimba kwanza mbele ya CDF wakati huo Gen David Musuguri ilikua Mgulani JKT ambapo alituelekeza tuurekodi haraka iwezekanavyo,tulitekeleza agizo lake na tuliurekodi.

3.Jeshi,Chama na Serikali waliupokeaje wimbo huo?

Jibu-Jeshi,Chama na Serikali vilifanya kazi kwa pamoja hivyo basi wimbo au kitu kikikubalika sehemu moja basi hakuna jinsi inakua kote imekubalika.

4.Hali ilikuaje kwa wananchi baada ya kuusikia  wimbo huo?

Jibu-Tumerudi kishujaa ni wimbo wa wananchi,shurani nyingi zimetolewa kwa wanajeshi wa JWTZ,JKT,Magereza,Polisi na FFU ya Polisi na bila kusahau wanajeshi wa Mgambo na wananchi wa kawaida waliojitolea kwa hali na mali kuukata uvamizi.
''dikteta kakimbia na Uganda katuachia na vita tumeshinda''

PATA MANENO YA WIMBO ''TUMERUDI KISHUJAA''

Zahir; Tulikua tupo Arua wazazi wetu ee X2
           Kwenye mipaka ya Uganda,na Nchi ya Sudan,
           Kwenye mipaka ya Uganda na Nchi ya Zaire
           Kwenye kijiji cha kobokoooo

Tukiwa tumemaliza kazi jukumu kubwa,mlotupa wetu wazazi kutoka Tanzania,kumfukuza msaliti,alovamia nchi yetu,na kumpa adhabu kisagondani ya mipaka yakeee.
Dikteta kakimbia na Uganda katuachia na vita tumeshinda ooo

           Tulikua tupo Arua wazazi wetu ee
            kwenye mipaka ya Uganda na Nchi ya Sudani,
            kwenye mipaka ya Uganda,na Nchi ya Zaire
            kwenye kijiji cha Koboko ,kijiji alichozaliwa fashist dikteta Idd Amin Dada oo

Ukatolewa mwito,wazazi munatwita wanenu,turudi nyumbani,
Makubaliano yakafanywa,mashujaa nusu wabaki,wakirekebisha mambo,
Tukiwa nusu tukaanza kufunga safari kurudi nyumbani

            Tulipofika Kampala,tukaaga jamaa
            Tulipofika Masaka,tukaaga jamaa,
            Tulipofika mbarara,tukaaga jamaa
Tulipofika Kagera tukakuta wazazi wetuee,kwa vifijo na shangwe,wanenu kutupokeaaa

Wazazi pamoja na sisi wanenu tukageuza vichwaa,kuitazama Uganda,
Na kuwaacha mashujaa wetu,walopoteza maisha,ndani,ya nchi ya Waganda,walikufa kishujaa oohh
            ooh wazazi

KIITIKIO; Wazaaazi,wazazi wetu eee
                   Wazaaazi,wazazi wetu eee
                   Mashujaa walokufa,wamekufa kishujaa,
                   Mashujaa tulorudi,tumerudi kishujaa,
Lengo na nia yetu wazazi ilikua moja,kuilinda ardhi yetu eee
kuilinda ardhi yetu eeeee  X 2

                   Kipindi kilopita wazazi wetu ee
                   Kipindi kilopita wazazi,kilikua kigumu
                   Kile kipind cha vita wazazi kilikua kigumu ee

                   Katika muda mfupi,tumeweza kujua,
                   Nani kwetu ni rafiki,
                   Nani kwetu ni hasidi,
                   Yalopita si ndwele wazazi,tugange yanayokuja,

                   Umoja wenye nguvu,
                   Mshikamano wa dhati,
                   Na nidhamu za hali ya juu,kwa wanajeshi wetueee,
                   Ndio siri kubwa,ya ushindi wetu wazazi wetu ee,
                   Na yote kwa pamoja,
                   Ni matunda halisi,ya siasa safi nchini mwetu na uongozi boraa,

              ooh wazazi

KIITIKIO; Wazaaazi,wazazi wetu eee
                   Wazaaazi,wazazi wetu eee
                   Mashujaa walokufa,wamekufa kishujaa,
                   Mashujaa tulorudi,tumerudi kishujaa,
Lengo na nia yetu wazazi ilikua moja,kuilinda ardhi yetu eee
kuilinda ardhi yetu eeeee  X 2


Saturday, July 16, 2016

KUMBUKUMBU YA MWAKA MMOJA TANGU BANZA STONE AFARIKI DUNIA, IMEANDALIWA NA DAUDI KISUGURU.

NI MWAKA MMOJA SASA UMETIMIA TANGU TASNIA YA MUZIKI WA DANSI
IONDOKEWE NA MWANAMUZIKI NGULI
RAMADHANI MASANJA "BANZA STONE"
Mwanamuziki huyu alifariki mwaka mmoja uliopita yaani mwaka jana  2015
kabla ya kifo chake mitaani kulitokea fununu mithili ya mchezo wa kuigiza pale watu walipokuwa wakizusha habari ya kuwa amefariki.

Pamoja na uzushi huo habari hizo zilikuwa zikikanushwa na familia yake hata na yeye mwenyewe kwa mapenzi ya mola ijumaa ya tarehe 17/07/2015 hii haikuwa uzushi tena bali ya mungu yasemayo kila nafsi itaonja mauti ikatimia banza stone aliaga dunia akiwa nyumbani kwao sinza jijini dar es salaam
alipokuwa akiuguzwa na kuzikwa siku iliyofuata ambayo ilikuwa jumamosi ya tarehe 18/07/2015 katika makaburi ya sinza kifo chake inasemekana kilitokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa saratani ya ubongo.

Ramadhani Masanja alimaarufu banza stone alizaliwa jijini dar es salaam tarehe 20/10/1972 akiwa mtoto wa tisa kati ya watoto kumi na moja ,alipata elimu yake ya msingi katika shule ya msingi MNAZI MMOJA ya hapahapa jijini dar es salaam ambako alianza darasa la kwanza mwaka 1981 na kuhitimu darasa la saba mwaka 1987 ,mara baada ya kumaliza shule ndipo alipoanza kujishughulisha na mambo ya muziki lakini akianza na muziki wa Hip hop enzi hizo ulikuwa ukisikilizwa kwenye radio tu akiwa na wenzake kama K - ONE na SCOS MAN hiyo ilikuwa mwaka 1989.

Mwaka 1990 akaanza mchakato mpya wa kunengua muziki wa dansi wa enzi hizo za miaka hiyo ya 1990 ambayo miziki ya congo ndiyo ilikuwa imetawala
"kwasakwasa" ,"nzawisa" n.k.

Walikuwa wakicheza sana kwenye maharusi yeye pamoja na wenzake YELLOW MAN na JESCA ONGALA mtoto wa DR REMMY.
Baada ya hii kuona hailipi ndipo alipoamua kujifunza muziki katika kituo cha utamaduni cha watu wa korea alikopelekwa na jirani yao aitwaye MZEE KAPIZO na kujifunza kupiga drums na bendi yake ya kwanza ilikuwa THE HEART STRINGS ,TWIGA ,AFRI - SWEZI na baadae akajiunga na ACHIGO BAND katika hizi alikuwa hamalizi hata mwaka ni miezi sita anaondoka.

Mnamo mwaka 1995 ndipo alitua THE AFRICAN STARS BAND wana twanga pepeta ikiwa bado changa kabisa ikiwa na mwaka mmoja tangu ianzishwe na kufanikiwa kurekodi nao albamu ya "kisa cha mpemba"sasa akiwa kama muimbaji.

Alihudumu ndani ya twanga pepeta kwa muda wa miaka mitano na kuachana nayo mwaka 2000 Banza stone aliihama african stars na kujiunga na TANZANIA ONE THEATRE ( T O T ). Wana achimenengule iliyokuwa ikiongozwa na KAPTENI JOHN KOMBA ambaye kwa sasa nae ni marehemu na kuweza kutunga nyimbo kama "mtaji wa masikini","elimu ya mjinga", akiwa hapa aliwahi kupata mafunzo ya muziki katika chuo cha sanaa bagamoyo. 

Mwaka 2003 aliachana na T.O.T. na kuanzisha bendi yake iliyokuwa ikifahamika kama BAMBINO SOUND bendi ambayo ilitoka na kibao matata kisemacho "miye niseme na wewe useme nani atamsikiliza mwenzie" kwa bahati mbaya bendi hii haikudumu ikasambaratika na yeye kurejea tena AFRICAN STARS  na baadae akajiunga na EXTRA BONGO, TWANGA CHIPOLOPOLO,
RUFITA JAZZ BAND.

Mwaka huo huo wa 2003 Banza alikuwa ni miongoni mwa wamuziki watatu walioshiriki kwenye zing zong iliyoandaliwa na mfadhili aitwaye MOHAMED MPAKANJIA mwingine ni ALLY CHOKI na MWINJUMA MUUMINI .
tutaendelea kumkumbuka kwa nyimbo zake zilizoibamba jamii enzi za uhai wake
kama "mtaji wa masikini" ,"elimu ya mjinga" ,"aungurumapo simba" ,"mtenda akitendewa" ,"falsafa ya maisha" ,"kumekucha" ,"mimi niseme nawe useme" ,"mshenga" na "sema unachotaka"

MUNGU AIWEKE ROHO YAKE MAHALI PEMA PEPONI NA AMPUNGUZIE ADHABU ZA KABURI - AMIN.