LATEST POSTS

Saturday, September 3, 2016

MUZIKI WA DANSI NI AJIRA YA WENGI,UKIYUMBA NA WENGI WANAYUMBA,ASEMA FAIDA ONGALA.



          MGENI WETU HII LEO NI FAIDA ONGALA WA AKUDO IMPACT


                                                Faida Remmy Ongala.

Blog pendwa ya Kavasha leo imepata bahati ya kukutana na mwanamuziki anaekuja kwa kasi ambae pia ni binti wa  mwanamuziki mkongwe wa miondoko ya dansi Marehemu Dokta Remmy Ongala,huyu si mwingine bali ni Faida Ongala,Kavasha Blog ilikua na machache iliyohitaji kujua toka kwake kwa ajili ya wasomaji wa wake na mazungumzo yalikua kama ifuatavyo;


1.Kavasha Blog;  Dada Faida wasomaji wa blog hii pote duniani wangependa kujua mawili matatu toka kwako,wewe ni nani na historia yako ya muziki mpaka sasa,bila shaka upo tayari kutujuza,karibu sana.

Faida;  Asante sana nipo tayari kuwajuza,Mimi naitwa Faida Remmy Ongala,ni miongoni mwa watoto wa Marehemu mwanamuziki Dokta Remmy Ongala,nilipenda muziki toka zamani nikiwa mdogo,nilivyomaliza masomo ya Sekondari nilijiunga na chuo cha muziki kiitwacho Evelyne Music School kilichopo Kimara bucha baada ya kusoma miezi mitatu nikahamia chuo cha DHW Country Music  Academy kilichopo Zanzibar baada ya kuona kuna unafuu wa ada,Nashukuru Mungu baada ya kuwa nafanya vema katika masomo nikapata wafadhili ambao walinisomesha bure kipindi chote ambachonilikua nikisoma hapo,nilisomea kupiga gitaa na ngoma za asili na kucheza pia na baada ya Chuo hicho cha Zanzibar nilikwenda Ethiopia ambapo nilisoma kwa miezi minane ambapo mpaka sasa nimemaliza masomo kwa jumla ya miaka mitatu ya masomo mbalimbali ya muziki kama nilivyoyataja katika vyuo vyote vitatu toka Dar,Zanzibar hadi Ethiopia.
                  Faida Ongala akifanya mazoezi nyumbani kwake.

2.Kavasha Blog;  oohh historia nzuri kabisa bila shaka ni mwanamuziki msomi Faida

Faida;anacheka….asante ni msomi kiasi ,yafaa sisi wanamuziki tupate elimu kidogo juu ya muziki ili kujua kwa undani muziki ukijumlisha na vipaji vyetu.

3.Kavasha Blog;  Ni nini ulichokipata kutoka kwa baba yako marehemu Dk Remmy Ongala kuhusiana na muziki?

Faida anajibu;Nimejifunza na kupata vitu vingi toka kwa baba angu mzee Remmy kama vile kufanya juhudi katika kazi yangu ya muziki  kitu ambacho nakifanya ili kuweza kufikia mafanikio yake yeye ama mara mbili zaidi ya pale alipofikia,kitu kingine alipenda kazi yake na mie pia ninaipenda kazi yangu katika mazingira na namna zote zile na kingine nimerithi kipaji chake cha muziki na kuwa mwanawe wa kike wa pekee niliye katika fani hii ya muziki. 


                           Baba wa Faida,Dr Remmy Ongala.

 4. Kavasha Blog;  Ni muziki gani unaumudu ?

Faida;Namudu miziki mingi na sipigagi miziki michache kama singeli,hiphop,taarab,michiriku nk.

5. Kavasha Blog;  Baba yako Dk Remmy alitumia kauli kali kutetea alichokiamini  mfano wimbo muziki asili yake wapi kuna maneno haya’’muziki sio uhuni,kama muziki ni uhuni kwa nini unanunua kaseti,unacheza muziki ama unaomba nyimbo redioni,je unawaambia nini wanaodhani muziki ni uhuni?

Faida; Ni kweli muziki sio uhuni,muziki ni kazi kama kazi nyingine na inapaswa kuheshimiwa na watu wasifikiri kuwa kila afanyae muziki ni muhuni la hasha,uhuni ni asili ya mtu ndio maana watu wanaofanya kazi katika ofisi zenye heshima utakuta ni wahuni,vizazi vya washika dini navyo utakuta kuna wahuni waliobobea na hata watoto wa matajiri wasio na shida ya chochote utakuta ni wahuni kupita wanamuziki hivyo napenda wadau wa muziki na wale walio nje ya muziki wafahamu kuwa muziki sio uhuni ni kazi nzuri na ya ujuzi mkubwa kama ama zaidi ya kazi ya baadhi ya wanobeza kazi ya muziki.

        Faida Ongala akijiandaa kupanda jukwaani Nchini Dubai.

6. Kavasha Blog;  Vipi kuhusu familia umeolewa?

Faida;Mimi sijaolewa na sina mtoto,ninaishi na familia yangu inayojumuisha mama na ndugu zangu wengine.
7. Kavasha Blog;  Uliwahi kufanya kazi na bendi ama makundi gani na sasa upo na  kundi gani?

Faida; Niliwahi kufanya kazi na kundi la kaka zangu Godfrey na Thomas katika Band yao inayojulikana kama Ongalas Band ,nikatoka kwa kaka zangu ili kujitafutia changu mwenyewe maana kutegemea cha ndugu sana ni tatizo na pia kuongeza uzoefu ambapo nilikwenda Dubai kujiunga na Band iitwayo 2extra Ngwasuma ambapo nimerudi na kujiunga na Band ya Akudo Impact vijana wa masauti,pia ninaweza kupiga kama solo artist,nimepita pia kundi la ndege watatu kwa muda mfupi.

               Hili ni kasha la wimbo wake wa UMEBADILIKA.

 8. Kavasha Blog;  Unaonaje maendeleo ya muziki hususani wa dansi nchini?

Faida; Kusema kweli muziki kwa hapa Tanzania umeshuka kiwango hasa muziki wa dansi,unajua muziki wa  dansi unategemewa na wanamuziki wengi na hata wasio wanamuziki kwa sababu unatoa ajira kwa watu wengi kwa wakati mmoja kuliko aina nyinginezo za muziki kama vile Bongofleva nk, hivyo muziki wa dansi unavyoendlea kushuka inakua mbaya sana kwa wanamuziki na wadau kwea namna moja ama nyingine.

9. Kavasha Blog;  Tangu kifo cha Mzee wako Dokta Remmy ile staili yake ya kutoa usia na kukemea maovu katika jamii na kupongeza wale waliofanya mazuri na wenye uthubutu hakika imepotea,ukiwa wa damu yake una mpango wa kufata nyayo zake?

Faida;Ndio nina mpango huo kwa sababu nilikua napenda alivyokua anawaambia ukweli watu na viongozi wazembe,mfano wimbo niseme nini ambao anasema ‘’saa mbili asubuhi,foleni kwenye supu,ofisi ipo na nani bwana weee’’ukiangalia wanamuzki wengi hasa wa kizazi kipya(bongofleva)wamejikita zaidi kwenye nyimbo za mapenzi lakini mimi nitafata nyayo za baba ili niweze kuelimisha wananchi katika jamii na walimwengu kwa ujumla kama alivyofanya baba.
          Marehemu Dokta Remmy Ongala wakati wa uhai wake.

10. Kavasha Blog;  Nini malengo yako ya baadae?

Faida anajibu; Natarajia kuwa mwanamuziki mkubwa sana kitaifa na kimataifa,pia niweze kufikia malengo yangu ninayoyawazia na kufanya vizuri katika tasnia hii ya muziki.
               Faida Ongala akipozi wakati wa mapumziko.

11. Kavasha Blog;  Unawaambia nini wadau,Serikali na wanamuziki kwa ujumla kuhusu kuinua muziki wa dansi na mingine kwa ujumla?

Faida anajibu;Jamani muziki wa dansi ni muziki wa toka enzi na enzi,umetumika sana katika shughuli za kitaifa na kimataifa kama wimbo Zimbabwe wa DDC Mlimani Park ukizungumzia uhuru wa Zimbabwe,naiomba serikali wajaribu kukaa na wadau wa muziki na wanamuziki kuangalia nini cha kufanya ili kurudisha hadhi ya muziki wa dansi nchini,pia nawaasa wanamuzki wote kuwa kitu kimoja bila kujali tofauti za makundi yao,ushrikiano ni jambo la msingi katika maendeleo yetu na pia kuupandisha muziki huu wa dansi.

Kavasha Blog;  Tunakushukuru Lady Doctor Faida Ongala kwa ushirikiano wako natumai tutaendelea kuwa pamoja siku zote.

Faida ;Asante na mie nafurahi kuzungumza na Blog ya kundi la Kavasha Group Tanzania.

                        KILA LA HERI DADA FAIDA ONGALA      
                ANAPATIKANA KWA SIMU NAMBA  ZIFUATAZO
                            +255715023646 KIKAZI ZAIDI.

0 comments:

Post a Comment