LATEST POSTS

Monday, August 8, 2016

MIAKA 12 BAADA YA KIFO CHA BALISIDYA,MFAHAMU KWA UFUPI.

KUMBU KUMBU YA MIAKA 12 TANGU KUFARIKI KWA MWANAMUZIKI MKONGWE NA MAHIRI NCHINI,MAREHEMU PATRICK MARTIN YOHANA BALISIDYA NA HISTORIA YA BENDI YA AFRO 70-IMEANDALIWA NA DAUDI KISUGURU.
 
                                                              Marehemu Balisidya.

Ni miaka kumi na mbili imepita tangu kufariki kwa mwanamuziki huyu mkongwe na mahiri katika tasnia hii ya muziki wa dansi aliyewahi kuvuma ndani na nje ya mipaka ya TANZANIA.

Ni mwanamuziki aliyekuwa anavimudu vyombo vingi vya muziki kama kinanda,gitaa zote,utunzi,uimbaji na upangaji wa muziki,PATRICK BALISIDYA ni mwenyeji wa mkoa wa Dodoma alizaliwa Mwezi April,1946 na kupata elimu yake ya msingi katika shule ya MVUMI BOYS PRIMARY SCHOOL waka 1954 na kushindwa kuendelea na masomo baada ya kuugua na kushindwa kufanya mtihani wa mwisho wa darasa la nne na baada ya matibabu ilibidi arudie ili aweze kufanya mtihani wa mwisho wa darasa la nne kwa bahati nzuri akafaulu na kuendelea na masomo ya darasa la tano mpaka la nane katika shule ya CHILONWA MIDDLE SCHOOL na baada ya mtihani wa darasa la nane akachaguliwa kuendelea na kidato cha kwanza katika shule ya DODOMA SECONDARY SCHOOL baada ya matokeo ya kidato cha nne PATRICK BALISIDYA alichaguliwa kujiunga na DAR ES SALAAM TECHNICAL COLLEGE ( Dar Tech) kwa sasa kinafahamika kama DAR ES SALAAM INTERNATIONAL TECHNOLOGY kwa ajili ya kuchukua Diploma ya majumba na umeme.

Harakati zake na hamasa ya kuupenda muziki inaanzia nyumbani kwao,Baba yake mzazi MZEE MARTIN YOHANA BALISIDYA alikuwa na gitaa la box galatoni ambalo alikuwa analipiga kwa kujifurahisha hapo nyumbani na mama yake mzazi alikuwa anapiga kinanda kanisani nae pole pole akaanza kujifunza na alijifunza zaidi pale alipojiunga na Dodoma secondary,Shule ilikuwa na bendi yake iliyofahamika kwa jina la CHITOMDULI ambayo PATRICK ndiye alikuwa anaiongoza.

Kwa haraka aliyokuwa nayo hapo aliona anachelewa kuyafikia malengo yake aliyokuwa nayo akawa anatoroka kwenda kushiriki na bendi ya CENTRAL JAZZ BAND iliyokuwa na maskani yake  hapo hapo mkoani Dodoma ambayo ilikuwa inamilikiwa na mbunge wa serikali yaTanganyika wakati huo aliyefahamika kwa jina la STANLEY MSUVE, hiyo ilikuwa ni Mwaka 1964 hali hii ikampelekea kuingia kwenye mgogoro kati yake na walimu wake mpaka kufikia kufukuzwa Shule,habari zilipowafikia wazazi ikabidi waingilie kati na hatimaye suluhu ikapatikana na Patrick kuweza kuhitimu kidato cha nne mwaka 1965.


Ujio wake katika Jiji la Dar es salaam kuja kujiunga na chuo cha DAR TECH ndiyo ikawa fursa kwake ya yeye kupata nafasi ya kujiunga na Bendi ya Dar es salaam jazz kikosi "B" na hatimaye kuwa kiongozi wa Bendi hiyo ya pili na ile ya kwanza yaani DAR JAZZ "A" ikiongozwa nae KING MICHAEL ENOCK.Bendi hii ikatoa upinzani wa hali juu kwa ile ya "A" na kupelekea uongozi wa juu wa Dar es salaam jazz band kuamua kumpandisha daraja Patrick kumtoa "B" na kumpeleka "A" hiyo ilipelekea kufanya kazi pamoja na KING ENOCK, King Enock akipiga solo namba moja na Patrick akipiga solo namba mbili.


Mwaka 1968 Dar es salaam jazz band ikaanza kufifia kutokana na uchakavu wa vyombo hali hiyo ikapelekea Patrick balisidya kuomba ridhaa kwa baba yake ili amsaidie kuanzisha bendi yake mwenyewe na baba yake akaafiki na kumnunulia Box gitaa nne na baadhi ya vyombo vingine walichukua vile vya iliyokuwa CENTRAL JAZZ BAND  ambayo kwa wakati huo ilikuwa imeshasambaratika na huo ndiyo ukawa mwanzo wa kuundwa kwa  AFRO 70 BAND "wana afrosa" Bendi ambayo ilipoanzishwa ilifahamika kama LES VOLCASE mwaka 1969 lakini haikupata usajili kwa sababu jina hilo lilionekana limekaa kizungu zaidi na haliendani na uasilia wetu. 


Ndipo mwaka mmoja baadae yaani mwaka 1970 kupitia watangazaji wa wakati huo hasa TIDO MUHANDO alikuwa akiwaita hao kuwa ni vijana wa AFRO mtindo wa nywele ulio kuwa maarufu kwa wakati huo na wao wakaongezea 70 wakaamua kujiita AFRO 70 wakitumia mtindo wa "afrosa" baada ya mazoezi makali bendi ikazinduliwa tarehe 25/12/1969 katika ukumbi wa STEREO NIGHT CLUB lakini Bendi ilianzia Tandika mtaa wa "sambwisi".


Ule umaarufu aliokuwa nao wakati akiwa na bendi ya Dar Jazz Band ulimsaidia kupata mapokeo mazuri kutoka kwa mashabiki katika siku hiyo ya uzinduzi, baada ya uzinduzi na kufanya maonyesho kadhaa ikabidi bendi isafiri kuelekea nchini KENYA kwa ajili ya kufanya recording ya nyimbo zao na kwenda kuingia mkataba na kampuni ya A.I.T. yaani ANDREW INTERNATIONAL TRADING na kufanikiwa kurekodi kwa lebo ya motomoto tarehe 23/05/1971 walirekodi nyimbo kama "vick" ," dirishani" ,"afrika" ,"bembea", "monika" ,"muongozo wa Tanu" n.k.

 
Patrick Balisidya -solo na kuimba ,second solo - Master Owen Franis Liganga , Rhythm - Jackson Makangila ,Besi - Charles George Matonya ,Ngoma - Saidi Nassoro ,Tumba -Hemedi Issa Kang'ombe wengine ni Zuberi Msekeni Didi , Teddy Chilufya,Salumu Munisi , Bille William Senzighwa na Adam Sykes na Steven Balisidya.

 
Tarehe 29/09/1971 walitoa vibao kama "mapenzi ya mama" ,"magreth" , "makayele", "kenya mpya" ," anjelina" na "pesa".Baadae wakahamia katika kampuni nyingine ya KELCHO  kwa OLUOCH KANINDO inayofahamika kama A.P.CHAMBRANE na tarehe 30/12/1971 walitoa vibao kama "libondela" ,"tembea tembea" ,"mpenzi Lidya" ,"Baba na Mama waheshimiwe" n.k.
Walitoa tena vibao vingine kama "gema" ," nataabika" ,"tausi" ,"mavula" ,"harusi" n.k. Hapa waliongezeka wanamuziki kama Shabani Mbotoni - sax, Paulo Ndasha - drum na Dickson Unga - mwimbaji na Tarehe 23/04/1972 walitoa nyimbo kama "nakupenda kama lulu" ,"ukombozi wa afrika" ,"dada yatubidi" ,"wapi heshima" na "kabla hujafa hujaumbika" na tarehe 15/07/ 1977 walitoa nyimbo kama "mashaka" ,"shangwe" ,"nini kisichokuwepo afrika" ,"week end" n.k.Pia waliongezeka wanamuziki kama, Sophia Nzuki ,Anna Mbula ,Rehema Kapteni , Habibu Jeff Mgalusi, John Festory, Christopher Phabbiano (Chriss Phabby ) na George Silvester.
 

Uwepo wa bendi hii katika tasnia ya muziki wa dansi katika miaka hiyo ya sabini unakumbukwa kwani iliwahi kunyakua ubingwa wa mashindano ya bendi za vijana yaliyowahi kufanyika jijini Dar es salaam mwaka 1971, 1972, 1973 na 1974, haya mashindano ndiyo yaliyowafanya kupata tiketi ya kuiwakilisha Nchi Nchini NIGERIA katika mashindano ambayo yalikuwa yafanyike mwaka 1975 lakini pakatokea mapinduzi ya kijeshi Nchini humo na mashindano kusogezwa mpaka mwaka 1977 yakihudhuriwa na bendi mbalimbali kama TP OK JAZZ, BEMBEA JAZZ BAND ya Guinea, AFRISA INTERNATIONAL, BELLAFONTE, ANEKOLAPO KUTI n.k. na AFRO 70 BAND ikiibuka na ushindi wa pili.

 
Tarehe 25/12/1975 wakati wanarejea kutoka ngerengere walikokwenda kufanya onyesho la kujitambulisha kwamba wao ndiyo wawakilishi  wa Nchi  Nchini Nigeria,walipata ajali pale Ubungo sehemu iitwayo ROMBO,gari waliokuwa wakisafiria ilipinduka na kupelekea vyombo vya bendi kuharibika vibaya na kuomba kujitoa katika mashindano hayo,lakini serikali kupitia kwa Waziri wa Wizara ya utamaduni wakati huo MIRISHO SARAKIKYA iliamua kuwapa vyombo ilivyokuwa imevinunua kwa ajili ya kuanzisha Bendi yake ili wawakilishe Nchi.


Baada ya kurejea nchini Nigeria kwenye mashindano yaliyofahamika kama maonyesho ya mtu mweusi Bendi ikapata mwaliko nchini MSUMBIJI  uliodhaminiwa na RADIO MOZAMBIQUE kwa wakati ule na kuweza kufanya maonyesho matatu kwa ajili ya wahanga wa vita vya kumng'oa MRENO na kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi 40,000/= pesa ya Msumbiji kwa wakati ule.


Waliporejea kutoka msumbiji wakatakiwa  AFRO 70 BAND wafanye onyesho la Chama na Serikali Patrick akadai malipo kwanza ndiyo afanye onyesho hali iliyopelekea kuingia kwenye mzozo mkubwa kati yake na serikali mpaka kupelekea kunyang'anywa vyombo, vyombo ambavyo ndivyo vilivyoanzishiwa bendi ya ASILIA JAZZ BAND naye Patrick Balisidya kufungua kesi ya madai mahakakani kesi ambayo inaendelea mpaka leo.
 

Lakini kwa bahati mbaya  Patrick alianza kusumbuliwa na maradhi yaliyopelekea kifo chake hapo Tarehe 08/08/2004 na kuzikwa tarehe 12/08/2004 katika makaburi ya Buguruni Malapa na kuiacha kesi yake ya madai mikononi mwa mdogo wake aitwaye FREEDOM BALISIDYA na huo ndiyo ukawa mwisho wa uwepo wa bendi ya AFRO 70 BAND na kutoweka katika ulimwengu huu wa tasnia ya muziki wa dansi.
 

Patrick Balisidya enzi za uhai wake baada ya AFRO 70 kutoweka aliwahi kufanyakazi na ORCHESTRA SAFARI SOUND "masantula"  na kupiga kinanda kwenye wimbo wa "niambie siri"  na THE RAIN BOW CONECTION Bendi iliyokuwa inapiga muziki wake pale NEW AFRICA HOTEL na Mwaka 1979 alienda Nchini SWEDEN na kufanikiwa kutoa albamu moja iliyoitwa "bado kidogo".
 
Patrick katika uhai wake aliwahi kufunga ndoa na BI SOPHIA NZUKI na walibahatika kupata mtoto mmoja wa kike aitwaye MAWANDO PATRICK BALISIDYA.

BWANA AMETOA NA BWANA AMETWAA.
 
JINA LA BWANA LIHIMIDIWE - AMIN.



                                                    R.I.P PATRICK BALISIDYA

0 comments:

Post a Comment